Thursday, July 2, 2020

NAIBU WAZIRI ULEGA ATEMBELEA VYAMA VYA USHIRIKA WA WAFUGAJI MKOANI TANGA

Muheza, Tanga

Naibu Wazir wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega jana Julai 01, 2020 ametembelea Vyama vya Ushirika wa Wafugaji wa ng'ombe wa maziwa katika wilaya ya Muheza mkoani Tanga.

Naibu Waziri Ulega katika ziara hiyo alikabidhi vibebea maziwa (cans) 50 kwa Chama Kikuu cha wafugaji Mkoani Tanga (TDCU) kwa ajili ya ubebaji maziwa.

Naibu Wazir wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega akikabidhi vibebea maziwa (cans) 50 kwa Wanaushirika wa Chama Kikuu cha wafugaji Mkoani Tanga (TDCU) kwa ajili ya ubebaji maziwa


Cans hizo zimetolewa na Marafiki wa Maendeleo, Heifer International kupitia program zake kusaidia ukusanyaji wa maziwa kutoka kwa vyama vya msingi vya wafugaji hadi kiwandani Tanga Fresh Ltd kwa Usindikaji ambapo cans hizi zitagawanya kwa vyama vya msingi wanachama wa TDCU.


Aidha, Naibu Waziri Ulega alikabidhi pia gari la kubebea maziwa kwa TDCU ambalo litasaidia kubeba maziwa ya wafugaji. Gari hilo kwa sasa litakuwa katika kituo cha Muheza na lingine linatarajia kufika mwezi Novemba,2020.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega akikabidhiwa gari la kubebea maziwa na Bw. Mac wa Heifer International kupitia program zake kusaidia ukusanyaji wa maziwa kutoka kwa vyama vya msingi vya wafugaji hadi kiwandani Tanga Fresh Ltd kwa Usindikaji. 


Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi na wanachama wa Vyama vya Ushirika wa Maziwa mkoani Tanga.


 Naibu Waziri Ulega pia katika ziara hiyo alikuja kujua kuhusu mafanikio na changamoto za mkopo wa TADB kwa mkoa wa Tanga kwa kuwa mkoa huo ndio ulikuwa wa majaribio (pilot) kwa mikopo ya TADB kwa Sekta ya Ufugaji. Kutokana na changamoto alizoelezwa, Mhe. Ulega alielekeza Wataalam wa Sekta Binafsi kukaa na TADB kutoa mwelekeo wa nini kifanyike kwa Mfugaji.


Naibu Wazir wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega akiwa na Wanaushirika mbele ya gari la ukusanyaji wa maziwa kutoka kwa vyama vya msingi vya wafugaji hadi kiwandani Tanga Fresh Ltd kwaajili ya Usindikaji.




WAKULIMA WATAKIWA KUWA NA VITAMBULISHO - WAZIRI HASUNGA

Chunya, Mbeya

Waziri wa Kilimo Mhe. Japhet Hasunga ametoa wito kwa wakulima nchini kuwa na Vitambulisho ili kurahisisha upatikanaji wa taarifa za mkulima kwa urahisi kama vile aina ya kilimo anachofanya, eneo analotoka, mazao anayolima na taarifa nyingine muhimu za utambulisho wake.

Waziri wa Kilimo Mhe. Japhet Hasunga, akizungumza kwenye hafla ya uzinduzi rasmi wa masoko ya minada ya Tumbaku wa mwaka 2020/21 uliofanyika Wilaya ya Chunya Mkoani Mbeya mwishoni mwa wiki iliyopita Juni 26, 2020

Waziri Hasunga aliyasema hayo wakati wa hafla ya uzinduzi rasmi wa masoko ya minada ya Tumbaku wa mwaka 2020/21 uliofanyika Wilaya ya Chunya Mkoani Mbeya mwishoni mwa wiki iliyopita Juni 26, 2020. Akifungua masoko hayo Waziri alisisitiza kuwa ni muhimu wakulima kuwa na vitambulisho kwani kilimo ni moja ya Sekta muhimu za uchumi wa Taifa letu kutokana na kilimo kuchangia pato la Taifa pamoja na  asilimia 30 ya fedha za kigeni kwa mahitaji ya kibiashara, ajira, chakula, na malighafi za viwandani.

Mrajis wa Vyama vya Ushirika, Dkt. Benson Ndiege, akizungumza kwenye hafla ya uzinduzi rasmi wa masoko ya minada ya Tumbaku wa mwaka 2020/21 uliofanyika Wilaya ya Chunya Mkoani Mbeya mwishoni mwa wiki iliyopita Juni 26, 2020

Katika hotuba ya ufunguzi huo, Waziri alitoa maelekezo kwa maafisa Ugani wafanye kazi zao kwa bidii wakizingatia kuwahudumia wakulima mashambani. Aliongeza kuwa maafisa ugani watumie muda wao mwingi mashambani ambapo ndipo wanapohitajika kutumia taaluma zao kuongeza uzalishaji wa kilimo chenye tija nchini.
“Kila mkulima asajiliwe, ajulikane yuko wapi analima kiasi gani, analima zao gani, analima ukubwa gani wa shamba, kiwango cha mavuno anachopata pamoja na changamoto alizonazo,” alisisitiza Waziri

Aidha, ameitaka Bodi ya Tumbaku nchini kuongeza kasi ya utafutaji wa masoko ya tumbaku inayozalishwa nchini kutokana na changamoto ya kupungua kwa wanunuzi wa zao la tumbaku pamoja na bei ya zao hilo kuendelea kushuka hivi karibuni. Jambo ambalo linasababisha kipato kwa wakulima kuathirika na mapato ya Serikali kupungua.

Mnada wa Tumbaku kwenye ghala la Chama cha msingi Lupa AMCOS

Pamoja na mambo mengine ameagiza Viwanda vya tumbaku visiuzwe bali vifufuliwe ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa azma ya Serikali ya kuendeleza na kuimarisha Uchumi wa viwanda, ambapo viwanda hivyo vitatumia mazao na malighafi za kilimo, kuongeza ajira na kukuza Sekta ya Viwanda.

Mrajis wa Vyama vya Ushirika Dkt. Benson Ndiege akizungumza katika uzinduzi huo amesisitiza Vyama vya Ushirika kuendelea kujikita katika kujenga na kuimarisha mitaji yake ya ndani ili kuwa na nguvu zaidi za kiuchumi katika Vyama itakayowezesha kukopesheka vizuri kwa riba nafuu kutoka kwenye taasisi za Kifedha na mabenki.

Dkt. Ndiege alieleza kuwa Tume ya Maendeleo ya Ushirika kwa kushirikiana na Serikali itaendelea kuchukua hatua dhidi ya wale wote watakaobainika kufanya shughuli za ushirika katika vyama bila kufuata taratibu au watumishi watakaokiuka maadili ya utumishi wa Umma, akimalizia kwa kuwaomba wadau kuendelea kutoa ushirikiano.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Umoja wa Wakulima wa Tumbaku (T.C.J.E), Bw. Emmanuel Charahani  katika maelezo yake amesema kuwa baadhi ya changamoto katika kilimo hicho ni kuendelea kuporomoka  kwa bei ya Tumbaku.  Akifafanua kuwa msimu wa 2016/17 wastani wa bei ulikuwa Dola 2.06 lakini msimu huu ambao soko la Tumbaku limefunguliwa bei ya wastani ni Dola 1.60. Hali inayopelekea wanunuzi na wakulima wa Tumbaku kuzidi kupungua na kuiomba Serikali kusaidia kunusuru hali hiyo kwa kutafuta wanunuzi zaidi wa Tumbaku.

Charahani amesema matarajio ya kitaifa ni kuzalisha kilo millioni 57 za tumbaku ambazo zinauzwa sasa, hii ikiwa imetokana na hali ya hewa mwaka huu ya mvua nyingi zilizosababisha mbolea kupotea ardhini.

Aidha, Mwenyekiti Charahani ameipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa jinsi inavyoendesha na kusimamia shughuli mbambali za kilimo kwa kutetea maslahi ya watu wanyonge. Ameipongeza pia Serikali kwa kuondoa baadhi ya tozo na kodi za Tumbaku ambazo zitasaidia kujenga hoja zenye nguvu katika kujadiliana bei ya Tumbaku na Wanunuzi.